KAMISHNA MSTAAFU WA MAGEREZA MAREHEMU EGNO KAMILIUS KOMBA

 

Marehemu Kamishna Mstaafu wa Magereza EGNO KAMILIUS KOMBA alizaliwa tarehe 20 Oktoba,1947 katika Kijiji cha Mtungu - Kindimba Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma.  Mwaka 1956 alijiunga na Elimu ya Msingi katika Shule ya Msingi Kindimba na kuhitimu elimu hiyo mwaka1959. Alijiunga na Shule ya Kati (Middle School) ya Litembo mwaka 1960 na kuhitimu mwaka 1963. Alijiunga na Shule ya Sekondari ya Kigonsera mwaka 1964 na kuhitimu Kidato cha Nne mwaka 1967.  Mwaka 1968 alijiunga na Shule ya Sekondari Karimjee iliyopo Mkoani Tanga na kuhitimu mwaka 1968.

Marehemu aliajiriwa na Jeshi la Magereza tarehe 02 Agosti, 1972 na kupelekwa kuhudhuria mafunzo ya awali ya Uaskari katika Chuo cha Usalama – Moshi. Marehemu alihitimu mafunzo hayo tarehe 30 Aprili, 1973 na kupangiwa kufanya kazi Gereza Malya, Mkoa wa Shinyanga.

Mwaka 1975 akiwa mwajiriwa wa Jeshi la Magereza, Kamishna mstaafu wa Magereza, Marehemu EGNO KAMILIUS KOMBA alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es salaam kwa ajili ya masomo ya Shahada ya Kwanza katika Uchumi  na kuhitimu mwaka 1978.

Marehemu akiwa Jeshini alitunukiwa vyeo mbalimbali kama ifuatavyo:-

Afisa Magereza  Daraja la III (PO III)– 30/04/1973 – 31/09/1973

Afisa Magereza  Daraja la I (PO I)- 01/09/1973 - 31/06/1976

Afisa Magereza Mkuu (PPO)-01/07/1976 - 30/11/1978

Mrakibu Msaidizi wa Magereza (ASP)- 01/12/1978 - 31/09/1980

Mrakibu Mwandamizi wa Magereza (SSP) - 01/10/1980 -31/12/1996

Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) - 01/07/1984 -19/09/1989

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP)-20/09/1989-30/6/1996

Kamishna wa Magereza (CP)   - 01/07/1996 - 30/06/2007 (Alipostaafu kwa umri Mkubwa).


Marehemu alifanya kazi katika vituo  vifuatavyo vya Magereza:-

Gereza Malya – Shinyanga - Tarehe 01/05/1973 - 12/05/1974

Makao  Makuu ya Magereza - Tarehe 13/05/1974 – 30/06/2007
                                                     

Katika utumishi wake Jeshini Marehemu pia alitunukiwa nishani mbalimbali kama ifuatavyo:-
• Nishani ya Mstari wa Nyuma ya Vita vya Kagera,
• Nishani ya Utumishi Mrefu Tanzania na,
• Nishani ya Utumishi Uliotukuka.

 

Katika utendaji wake wa kazi, Marehemu alikuwa na uwezo mkubwa wa kujifunza, kutawala na kuyamudu majukumu yake ya kazi ipasavyo.  Viongozi na watumishi wa Jeshi la Magereza tunamlilia mno kwa Utumishi wake uliotukuka na hazina kubwa ya utendaji aliyoondoka nayo  kwani hata baada ya kustaafu katika Jeshi la Magereza bado alikuwa akitoa ushauri katika mambo mbalimbali ya Uendeshaji wa Jeshi la Magereza.


Kamishna Mstaafu wa Magereza EGNO KAMILIUS KOMBA alikuwa anasumbuliwa na Ugonjwa wa Moyo hadi umauti ulipomkuta mchana ya tarehe 31 Julai, 2016 nyumbani kwake Mvuti, Chanika Jijini Dar es Salaam. Mwili wa Marehemu unatarajiwa kuzikwa kesho Agosti 3, 2016 Shambani kwake Mvuti, Jijini Dar es Salaam.

 
MWENYEZI MUNGU AIWEKE PEMA PEPONI ROHO YA MAREHEMU EGNO KAMILIUS KOMBA, AMEN