Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike akisalimiana na Mkuu wa Gereza Songwe, SSP. Peter Anatory alipowasili katika Gereza la Kilimo Songwe leo januari 25, 2019 kwa ziara ya kikazi ya kukagua utendaji kazi wa Jeshi hilo pamoja na kukagua mashamba ya kimkakati katika kuelekea kujitosheleza kwa chakula cha wafungwa magerezani.

 

Na ASP Lucas Mboje, Mbeya
KAMISHNA Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike amesema kuwa Jeshi la Magereza limeanza utekelezaji wa mpango wa miaka mitano wa kuelekea kujitosheleza kwa chakula cha wafungwa magerezani katika magereza kumi (10) ya kimkakati likiwemo Gereza Songwe, lililopo Mkoani Mbeya ambalo limelima hekari 750 za zao la mahindi.

Akizungumza na wanahabari leo mara baada ya kukagua mashamba ya mahindi katika Gereza la Kilimo Songwe, Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike amesema kuwa lengo la ziara yake ni kujionea hali halisi ya ufanikishaji wa jukumu walilopewa na Serikali katika kuhakikisha kuwa wanazalisha chakula kwa wingi cha wafungwa waliopo magerezani.

Amesema kuwa Mkoa wa Mbeya ni miongoni mwa mikoa ambayo imeingizwa katika utekelezaji wa mpango huo wa uzalishaji chakula cha wafungwa ambapo kila Gereza la kimkakati limepangiwa malengo ya kulima mazao mbalimbali ya chakula cha wafungwa ikiwemo mahindi, maharage na mpunga.

“Mpango huu ni lazima tuufanikishe, hivyo tayari tumekwishajipanga na nguvu kazi ya wafungwa inatumika ipasavyo katika kufanya kazi katika magereza hayo kama mlivyojionea leo hapa Gereza Songwe, pia tunajitahidi kusimamia rasilimali nyinginezo tulizonazo katika maeneo yetu ya magereza ili tuweze kutekeleza ipasavyo maelekezo ya Serikali”. Alisisitiza Jenerali Kasike.

Aidha, Jenerali Kasike ameongeza kuwa kwa sasa Jeshi hilo linakusanya rasilimali zilizopo na kutoa kipaumbele katika magereza yakimkakati, ambapo katika kukidhi mahitaji ya nguvu kazi ya wafungwa, tayari wafungwa kutoka sehemu mbalimbali nchini wamehamishiwa katika magereza yenye mkakakati ili kuongeza nguvu kazi yakutosha katika maeneo hayo yenye uzalishaji.

Akisoma taarifa ya Magereza Mkoa kwa Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Mkuu wa Magereza Mkoani Mbeya, SACP. Luhende Makwaia amesema kuwa Mkoa huo una jumla ya magereza matano ambayo yanatekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwemo miradi ya kilimo, likiwemo Gereza Songwe.

Kuhusu msongamano wa wahalifu, SACP. Luhende Makwaia amesema kuwa magereza yote ya mkoa wa mbeya yanakabiliwa na tatizo la msongamano wa wafungwa na mahabusu kutokana na ongezeko la uhalifu unaotokana na kuongezeka kwa idadi ya watu pamoja na kukosekana kwa gereza moja la wilaya katika mkoa huo.

Mkoa wa Mbeya una jumla ya wilaya sita(6) ambazo ni Mbeya mjini, Mbeya Vijijini, Chunya, Rungwe, Mbarali, na Kyela. Katika wilaya hizo ni wilaya tano(5) tu zina magereza, wilaya moja(1) ya chunya hakuna gereza hali inayochangia uwepo wa msongamano wa wahalifu katika mkoa. Aidha, katika magereza matano yaliyopo hupokea na kuhifadhi wafungwa na mahabusu katika mkoa huo.

 

Kwa habari picha zaidi tembelea www.magereza.blogspot.com