Na Lucas Mboje, Dar es Salaam
KAMISHNA Jenerali wa Magereza nchini, Dkt. Juma Malewa(pichani) ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kufanikisha mchakato wa ununuzi wa magari 450 ya Jeshi hilo ambayo yanatarajiwa kupokelewa muda wowote kuanzia sasa.

Kamishna Jenereli Malewa ameyasema hayo leo katika ufunguzi rasmi wa mkutano wa wakuu wa  magereza yote Tanzania Bara unaofanyika kwa siku moja katika Bwalo kuu la Maafisa magereza, ukonga jijini Dar es Salaam.

Jenerali Malewa amesema kuwa upatikanaji wa magari hayo utapunguza tatizo kubwa la uhaba wa magari kwa ajili ya shughuli za uendeshaji na utawala pamoja uboreshaji wa utekelezaji wa majukumu ya Jeshi hilo.

“Nichukue nafasi hii kumshukuru kwa dhati Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na serikali yote kwa ujumla kwa namna inavyoshughulikia utafutaji wa ufumbuzi wa changamoto tulizonazo,” alisema Jenerali Malewa.

Aidha kuhusu madeni ya Watumishi wa Jeshi hilo na wazabuni, Kamishna Jenerali Malewa amesema serikali imetoa kiasi cha zaidi ya Bilioni 8 za pesa ya kitanzania kwa ajili ya kulipa madeni hayo ambapo madeni yote yaliyokwisha kuhakikiwa tayari yameanza kulipwa na wahusika wamekwishaanza kupata fedha wanazodai Jeshi hilo.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Mhandisi Hamad Yusuph Masauni akizunguza katika ufunguzi wa Mkutano huo ametoa rai kwa jeshi hilo kutumia vyema fursa zilizopo katika katika maeneo mbalimbali ya jeshi hilo kwa kuanzisha na kuimarisha viwanda vidovidogo vilivyopo ili kuongeza uzalishaji hivyo kuchangia pato la taifa.

Masauni amesema kuwa Jeshi la Magereza linazo fursa nyingi sana za uzalishaji yakiwemo maeneo makubwa yanayofaa kwa kilimo, miradi ya ufugaji na miradi mengineyo ya kiuchumi.

“Nisisitiza kwamba wekeni mikakati yenye lengo la kuongeza uzalishaji katika maeneo yenu kwani nataka kila mmoja wenu katika gereza alilopo aweke malengo ya kuongeza uzalishaji kulingana na fursa zilizopo,” alisema Mhe. Masauni.

Mkutano huu wa Wakuu wa Magereza yote Tanzania Bara unajumuisha Maafisa Waandamizi kutoka Makao Makuu ya Magereza na Wakuu wa vituo vya Magereza yote nchini ambapo lengo kuu ni kujadiliana kwa kina hali halisi ya utendaji kazi magerezani na kuweka mikakati ya kukabiliana na changamoto zilizopo ili kuongeza tija na ufanisi. Kauli mbiu ya mkutano huo ni JESHI LA MAGEREZA KATIKA JITIHADA ZA KUFANIKISHA KUELEKEA TANZANIA YA UCHUMI WA VIWANDA.