UJUMBE KUTOKA KWA KAMISHNA JENERALI WA MAGEREZA NCHINI |
Jeshi la Magereza lipo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na lilianzishwa rasmi kama idara inayojitegemea mnamo tarehe 25 Agosti, 1931. Kabla ya kuanzishwa kwake utekelezaji wa majukumu yake ulikuwa unafanyika kwa pamoja na Jeshi la Polisi. Lengo kuu lilikuwa kuwalinda wafungwa wasitoroke na kuwafanyisha kazi ngumu wafungwa waliohukumiwa. Pamoja na Jeshi hili kujitenga, utendaji haukubadilika sana hasa katika kuwahudumia wafungwa na mahabusu kwani lengo kuu lilibaki lilelile la kuwalinda wafungwa wasitoroke, na kuwafanyisha kazi ngumu. Baada ya uhuru tarehe 9 Desemba, 1961 utendaji wa kazi ulibadilika kwa kuingiza fikra mpya katika uendeshaji wa magereza ambapo pamoja na mambo mengine masuala ya haki za binadamu yalizingatiwa katika kuwahudumia wafungwa na mahabusu na dhana ya urekebishaji ilianza kushika kasi. Mabadiliko haya yalipewa nguvu za kisheria kwa kutungwa kwa sheria ya Magereza ya mwaka 1967, iliyowezesha kutungwa kwa Kanuni, Miongozo na taratibu mbalimbali katika uendeshaji wa Jeshi la Magereza. Sheria hiyo pamoja na mambo mengine zilizingatia mikataba mbalimbali ya Kimataifa ya haki za binadamu katika utunzaji na uhudumiaji wa wafungwa. Jeshi la Magereza ni mojawapo ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama. Majukumu yake ni kuchangia katika kuleta, kuendeleza na kudumisha usalama wa jamii nchini kwa kufanya yafuatayo:- i) Kuwahifadhi wafungwa wa aina zote wanaowekwa gerezani kwa mujibu wa sheria; ii) Kuandaa na kutekeleza programu za urekebishaji wa wahalifu kwa kuwafundisha shughuli mbalimbali za uzalishaji na ujuzi kwa njia ya vitendo na ushauri; iii) Kuendesha shughuli na huduma kwa wafungwa kwa mujibu wa Sheria; iv) Kuchangia katika ushauri kuhusu uzuiaji na udhibiti wa uhalifu na urekebishaji. Pamoja na majukumu hayo Jeshi la Magereza vilevile hutoa wataalam wake wenye fani mbalimbali ili kusaidia kuimarisha mpango wa Umoja wa Mataifa wa Kulinda Amani (United Nations Peacekeeping Mission – UNPM). Pamoja na changamoto mbalimbali zinazolikabili Jeshi letu, namshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete ambaye ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama pamoja na Serikali kwa ujumla kwa jitihada zake mbalimbali za kuendelea kulijengea uwezo Jeshi letu kwa kulipatia rasilimali fedha na watu, vitendea kazi katika kutekeleza majukumu yetu ipasavyo. |
. |