TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Tarehe 21 Oktoba, 2016 saa 3:00 asubuhi Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi, Mhe. Balozi Hassan Simba Yahya anatarajia kuwa mgeni rasmi kwenye sherehe za mahafali ya 13 ya Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari ya Bwawani iliyopo Mkoa wa Pwani.

Shule ya Sekondari Bwawani inamilikiwa na Jeshi la Magereza, ilianzishwa mwaka 1978 kwa lengo la kutoa elimu ya Sekondari kwa Watumishi wa Magereza ambapo hivi sasa Shule hiyo inatoa elimu ya Sekondari kwa vijana wa kike na kiume kutoka maeneo mbalimbali hapa nchini.

Shule hiyo pia inatoa elimu ya Kidato cha Tano na Sita, katika muunganiko wa masomo ya Historia, Jiografia na Kiswahili (HGK), Historia, Jiographia na Kiingereza(HGL). Aidha, mwaka huu inatarajia kuanzisha mkondo wa masomo ya sayansi(CBG) yaani masomo ya Kemia, Baiologia na Jiografia.

Jumla ya Wanafunzi 94 wa shule hiyo wanatarajia kuhitimu elimu yao ya kidato cha nne  mwezi Novemba mwaka huu.

Sherehe hizo zitajumuisha mambo yafuatayo:-

- Mgeni rasmi kutembelea maeneo ya shule na kuweka mawe ya ufunguzi katika majengo ya shule
- Mgeni rasmi kuangalia Maonesho ya Taaluma kwa Wanafunzi Washiriki;
- Mgeni rasmi kutoa vyeti na zawadi mbalimbali kwa Wanafunzi wahitimu na;
- Mgeni rasmi kutoa hotuba

Sherehe za mahafali hayo zinatarajia kukamilika saa 8:00 mchana. Vyombo vya Habari vinakaribishwa kwenye sherehe hizo tarehe 21 Oktoba, 2016 kuanzia saa 3:00 asubuhi.

Imetolewa na: Lucas Mboje,
Mrakibu Msaidizi wa Magereza,
Afisa Habari wa Jeshi la Magereza,
DAR ES SALAAM

20 Oktoba, 2016.